1YOHANA 5:8 NA MATHAYO 28:19 ZINASEMAJE?
1. 1YOHANA 5:8
"Kwa maana wako watatu washuhudiao Mbinguni Baba na neno
na roho mtakatifu na watatu hawa ni umoja"(1yohana 5:8)
Kwa kuanza kabisa, mstari huu ni mstari
maarufu sana na unatumiwa kama ndio mstari mkuu unaoonesha kuthibitisha kuwa
Mungu ni nafsi tatu. Lakini kwa mtu yoyote yule ambaye ni mwaminifu wa moyo na
moyo wake hauna mabishano atajiuliza kwanini katika Mistari mingi ya Biblia
Mungu mwenyewe anashuhudia kuwa yeye ni nafsi moja afu mstari mmoja huu ndio
ubadili maana nzima ya Mungu mwenyewe? Na kuna watu japokuwa umetoa mistari
mingi ya biblia kuonesha kuwa Mungu ni mmoja lakini bado anatumia mstari huu
kutokukubali ukweli wa biblia hata kuifumbia macho mistari ya wazi inayoonesha
kuwa Mungu ni nafsi moja tu. Sasa taratibu na tuangalie mstari huu kwa kina.
Katika mstari huu msomaji na angalie vizuri. Je katika mstari huu wapi
panaposema Mungu ni nafsi tatu? Au wapi panaposema kuwa Baba, mwana na Roho ni
nafsi tatu za Mungu? Hata wewe msomaji unaona wazi kuwa Mstari hausemi chochote
kuhusu Mungu kuwa na Nafsi tatu. Sasa kama mstari hausemi Mungu ananafsi tatu
kwa nini tudhani Mungu ni nafsi tatu?
Mstari umesema wazi Kuwa Baba mwana na Roho ni umoja. Na umoja wao ni katika
ushuhuda ule wanaotoa. Hichi ndicho mstari huu unasema. Tujiulize Nini maana ya
neno umoja? Je watu wakiwa na umoja wanaungana na kuwa kiumbe chenye nafsi
nyingi au wanakuwa katika hali ya kupatana na kunia mamoja? kwa mfano, umoja wa watu watatu unawafanya
waungane na kuwa mtu mmoja katika nafsi tatu? Je ikiwa mimi wewe na yule
tunaumoja, Je miili yetu inaungana na kuwa mwili mmoja wenye nafsi tatu? Sasa
kwanini nauliza haya maswali? Ni ili tuweze kutafakari nini maana ya umoja kwa
maana ile ile tunayotumia katika mazingira ya kila siku. Tuangalie mfano
"Kwa hiyo mwanaume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana
na mkewe nao watakuwa mwili mmoja"(Mwanzo 2:24)
Katika ndoa Je mwanaume na mwanamke wanaungana na Kuwa Mwili mmoja wenye
nafsi mbili? Hapana. Bali umoja wao ni katika kupendana, kutunzana, Na kunia
mamoja lakini kamwe hawawezi kuungana na Kuwa mwili mmoja mwenye nafsi mbili.
Hata msomaji ni shahidi kuwa hakuna ndoa inayowafanya wanandoa waungane na kuwa
Mtu mmoja katika nafsi mbili. Tuangalie mfano mwingine
“Wote wawe na umoja kama wewe Baba ulivyo ndani yangu, nami ndani yako, hao
nao wawe ndani yetu ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe
uliyenituma.”(Yohana
17:21)
Yesu aliwaombea wanafunzi wake kumi na mbili wawe na umoja kama jinsi yeye
Yesu na Baba yake walivyo na umoja hivyo umoja wa mitume ndio umoja ule ule
kati ya Baba na mwana. Sasa tujiulize je umoja wa wanafunzi 12 wa Yesu
unawafanya waungane na kuwa mtume mmoja katika nafsi 12?. Hapana kila mtume ni
nafsi huru. Sasa Yesu aliposema umoja alikuwa anamaana umoja wa aina gani?
Hata na sisi sote tutakapoufikia Umoja wa imani na kumfahamu sana
mwana wa Mungu, hata kuwa mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha
utimilifu wa Kristo
(Waefeso 4:13)
Yesu alikuwa anawaombea wanafunzi wake wawe na umoja wa imani. Katika
kumuamini Yesu Kristo.Watu waliokatika kanisa moja wanaumoja katika Imani,
Umoja wao hauwafanyi wawe mwili mmoja katika nafsi nyingi. Lakini kitu cha
kushangaza ni kwamba unapokuja katika umoja wa Baba na Mwana na Roho watu
wanaanza kumaanisha kuwa hawa watatu wanaungana na kuwa nafsi tatu kitu ambacho
hata biblia haisemi kuwa Mungu ni nafsi tatu wala hakuna wanafunzi wa Yesu
walioungana na kuwa Mtume mmoja katika nafsi 12. Tunajua kuwa umoja wa
Wanafunzi wa Yesu ndio umoja kati ya Baba na Mwana, lakini kwa upande wa
wanafunzi wa Yesu, umoja wao hauwafanyi waungane na kuwa mtume mmoja katika
nafsi 12, lakini kwa upande wa Baba mwana na Roho umoja huo unawafanya waungane
na kuwa mmoja katika nafsi tatu jambo ambalo linashangaza sana. Tunasahau kuwa
umoja wao ni katika ushuhuda. Kama imetokea ajali walioshuhudia ile ajali
wanatoa maelezo mamoja ushuhuda huu unawafanya wawe ni umoja . Je ushuhuda wa
watu walioona ajali fulani unawafanya wawe mwili mmoja katika nyingi? Hapana
kila mmoja ni Nafsi inayojitegemea na hakuna muunganiko wowote. Sasa Mungu
mwenyewe amesema yeye ni Nafsi ngapi?
"Akasema Nimeapa kwa NAFSI YANGU asema BWANA kwa kuwa umetenda neno
hili wala hukunizuilia mwanao mwanao wa pekee"( Mwanzo 22:16)
kama Mungu angekuwa ni zaidi ya nafsi moja kwanini anasema Nimeapa kwa
"NAFSI YANGU" au je neno hili huwa linatumika pale ambapo nafsi
zinakuwa nyingi? Kama Mungu angekuwa ni zaidi ya nafsi moja Basi angesema
Ameapa kwa Nafsi "ZAKE" lakini
hapana Mungu anashuhudia kuwa Yeye ni nafsi moja tu. Mstari mwingine
"Tazama mtumishi WANGU nimemtegemezaye mteule WANGU ambaye NAFSI YANGU
imependezwa naye nimetia roho YANGU juu yake naye atawatolea mataifa hukumu"( isaya 42:1).
Tazama jinsi Mungu mwenyewe anavyojishuhudia kuwa yeye Ni nafsi Moja tu.
Sasa kati ya watatu hawa washuhudiao
mbinguni nani ni Mungu?
"Na ahimidiwe Mungu, Baba Wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema
Mungu wa Faraja yote"(
2wakorintho 1:3)
Sasa tunaelewa kuwa Umoja wa Baba na Mwana na Roho katika mstari huu
hauwafanyi waungane na kuwa mmoja katika nafsi tatu, bali umoja wao ni katika
Ushuhuda wanao utoa, Ushuhuda wa Baba ni sawa na ushuhuda wa Mwana na ushuhuda
wa Mwana ni sawa na ushuhuda wa Roho na ushuhuda wa Roho ni ushuhuda wa Baba na
mwana. Hii ndio maana halisi ya umoja. Hivyo basi japokuwa Baba Mwana na Roho
ni Umoja katika ushuhuda, Baba ndiye Mungu ambaye Biblia imemtaja.
Kwa upande mwingine mstari huu haukuwepo katika maandiko halisi ya Mtume
Yohana maneno hayo yaliingizwa baadae ili kuunga mkono fundisho la utatu. SDA
bible commentary imesema kuwa,
Kifungu hiki kama kinavyoonekana katika KJV hakipo katika nakala yoyote ya
kigiriki kabla ya karne ya 15 na 16. Maneno haya yasiyokubalika yalipata njia
kuingia katika KJV kwa kupitia Maandiko ya Kigiriki ya Erasmus (Ona Vol. V
p.141). Inasemekana kuwa Erasmus alitaka kuingiza maneno haya yasiyokubalika
katika Maandiko yake kama angeoneshwa hata nakala moja inayoonesha kuwepo na
maneno hayo. Maktaba ya Dublin imetengeneza Nakala kama hiyo (Inajulikana kama
34) na Erasmus aliingiza kifungu hicho katika maandiko yake. Sasa inaaminika
kuwa matoleo ya baadaye ya Vulgati yalipata kifungu hiki kwa makosa ya
mwandishi aliyeyaingiza kimakosa katika
maandiko ya biblia ambayo alikuwa ananakiri. Maneno haya yasiyokubalika
yamekuwa yakitumika sana katika kuunga mkono fundisho la utatu, lakini katika
kuangalia ushahidi wa kushtusha unaopinga uhalali wake, kukubalika kwake
umekuwa ni kiasi kidogo na huwa hayatumiki. Japokuwa yanaonekana katika Vulgati
tafsiri ya kikatoliki kuhusu Maandiko matakatifu ni wazi inakubali kuhusu
maneno hayo “sasa inaaminika kwamba kifungu hichi ambacho sasa kinaitwa Comma
Johanneum iliingia katika maandiko ya kale ya kilatini na Vulgati, Yalipata
upenyo kuingia katika maandiko ya kigiriki katika karne ya 15 na 16 (SDA Bible Commentary vol. 7 675)
Ni wazi kuwa maneno hayo yaliingizwa katika Biblia lakini hayakuwa ni
maneno halisi yaliyoandikwa na mtume Yohana, maneno haya yaliingia ili kuunga
mkono Fundisho la utatu ambalo halina misingi yoyote kutoka katika maandiko.
Ili kwamba ionekane kuwa fundisho hili ni la Biblia waliingiza maneno hayo ili
kuonesha kuwa fundisho hili lipo katika bibia.
2. MATHAYO
28:19.
“Basi enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi mkiwabatiza kwa jina
la Baba na mwana na Roho mtakatifu”(Mathayo 28:19)
Kila mmoja ni mwanafunzi wa Kristo kama Kristo anaishi ndani yetu. Kama
roho wa kristo anaishi ndani yetu, basi sisi tu wanafunzi wa Kristo. Kristo
anawaambia wanafunzi wake kuwa enendeni duniani kote kuwafanya mataifa yote
kuwa wanafunzi wake. Kila mmoja anajukumu la kuleta watu kwa Kristo. Kila mmoja
ana kazi ya kufanya kuhakikisha wanaokombolewa ni wengi. Sasa mstari unasema
kuwa, hawa wanafunzi wabatize kwa jina la Baba la mwana na la Roho mtakatifu.
Kila mmoja anayefika hapa inabidi awe makini sana ili kuona maana halisi
inayozungumziwa hapa. Mara nyingi wanafunzi wa Biblia wanapofika hapa wanasoma
huu mstari kama vile unathibitisha kuwepo kwa utatu.
Sasa tuangalie kwa umakini huu mstari na tuone je unathibitisha kuwepo kwa
utatu au la? Kwanza kabisa msomaji arudie kusoma tena huu mstari. Baada ya
kusoma tena huu mstari msomaji na ajiulie je katika mstari huu, ni wapi
panaposema kuwa Baba, mwana na Roho mtakatifu ni nafsi za Mungu? Au ni wapi
panaposema kuwa Baba mwana na Roho wanaunda Mungu mmoja? Mstari hausemi kabisa
hayo lakini mara nyingi tunaposoma Biblia tunakuwa na maana yetu kichwani
ambayo sio sahihi. Mstari huu umesema wazi kuwa mataifa wakabatizwe kwa jina la
Baba na Mwana na Roho mtakatifu, hausemi hata kidogo kuwa “Mungu ana nafsi tatu”.
Hata msomaji ni shahidi kuwa mstari hausemi kuwa Mungu ni nafsi tatu. Sasa kama
mstari hausemi kuwa Mungu ni nafsi tatu. Kwanini sisi leo hii tunautumia kama
ndio mstari mkuu unaothibitisha kuwa Mungu ana nafsi tatu wakati mstari wenyewe
hausemi hilo? Mstari huu umetafsiriwa Vibaya na wengi, na wengi hawajui jinsi
gani mstari huu umetafsiriwa kuthibisha kitu ambacho hakipo katika Biblia. Hivyo
kwa ufupi kabisa msomaji ni shahidi kuwa mstari hausemi kuwa Mungu ni nafsi
tatu, wala hausemi kuwa Baba,mwana na Roho wanashirikiana kuunda Mungu mmoja
mwenye nafsi tatu.
Pia mstari umesema kuwa Ubatizo ni kwa jina la Baba na Mwana na Roho
mtakatifu tulinganishe na mistari mingine katika Biblia
“Akaamuru wabatizwe kwa jina lake Yesu Kristo. Ndipo wakamsihi azidi
kukaa siku kadha wa kadha”
(Matendo 10:48)
“Waliposikia
Haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu” (Matendo 19:5)
Kwa maana na bado hajawashukia hata
mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu” (Matendo 8:16)
“Petro akawaambia Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo,
mpate ondoleo la dhambi zenu nanyi mtapokea kipawa cha Roho mtakatifu”( Matendo 2:38).
Katika Mistari hii tuliyosoma utagundua kuwa mitume walibatiza kwa jina la
Kristo. Ubatizo ulikuwa kwa jina lake Yesu Kristo. Lakini tunaposoma Mathayo
28:19 tunaona kuwa ubatizo ni kwa jina la Baba na Mwana na Roho mtakatifu.
Swali linaibuka je katika Ubatizo inabidi tubatizwe kwa jina la Yesu au kwa
jina la Baba mwana na Roho mtakatifu? Ili tupate jibu zuri inabidi tuchuguze
vizuri maandiko biblia inasema,
Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo
kila Jina, ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe la vitu vya mbinguni na
vya duniani na vya chini ya nchi na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI
BWANA kwa utukufu wa Mungu Baba” (Wafilipi 2:9-10).
Ni wazi kuwa hakuna Jina lililo kuu kuliko Jina la Kristo. Hakuna jina
ambalo limetukuzwa Mbinguni na duniani kuliko jina la Kristo. Jina la Yesu
ndilo Jina kuu kuliko majina yote juu mbinguni na hata chini duniani hata chini
ya dunia. Yesu Mwenyewe ana shuhudia kuwa
“Yesu akaja kwao akasema nao akawaambia, Nimepewa mamlaka yote
mbinguni na duniani”(Mathayo
28:18)
Yesu Kristo anashuhudia kuwa amepewa mamlaka Yote juu mbinguni na chini
Duniani. Ni sahihi pia kusema kuwa Jina la Yesu ndio Jina lenye mamlaka yote
juu mbinguni na chini duniani. Kwajina la Yesu kila jina litapiga goti na
kukiri kuwa Yesu ni BWANA. Yesu alisema
Yesu akasema Mimi ndimi njia na kweli na uzima mtu haji kwa Baba ila kwa
njia ya mimi (Yohana 14:6)
Kama hakuna mtu anaweza kwenda kwa Baba bila kupitia kwa Kristo ni sahihi
kusema kuwa hakuna mtu yoyote ambaye anaweza kwenda kwa Baba bila Jina la
Kristo. Bila jina la Kristo hakuna mtu ambaye anaweza kuokolewa. Jina la Kristo
ndilo njia pekee ya mtu kuokolewa. Hivyo mistari hii imeweza kujibu swali letu
kuwa ni Jina la Kristo tu ndilo Jina lililo bora kuliko majina mengine yale.
Tunajifunza kuwa imempendeza Baba kuwa Jina la mwanae Yesu Kristo liwe jina
kuu, kuliko majina mengine mbinguni hata kuliko Jina lake mwenyewe. Baba ameona
Jina la mwana wake liwe jina zaidi hata lake huko juu mbinguni.
Sasa swali Jingine linaibuka kuwa kama Ubatizo unatakiwa kuwa kwa kupitia
jina la Kristo kwanini Mathayo 28:19 imesema ubatizo ni kwa jina la baba na
mwana na Roho mtakatifu? Na kwanini mstari huu usomeke tofauti na mistari
mingine?
Ni kwa sababu kanisa katoliki lilibadili mstari huu wa biblia kutoka
kusomeka kuwabatiza kwa jina la Yesu Kristo mpaka kusomeka kuwabatiza kwa jina
la Baba na mwana na Roho mtakatifu. Ushahidi upo wazi kutoka katika kitabu cha
kikatoliki cha Catholic Encyclopedia inasema
“Kanuni ya ubatizo ilibadilishwa kutoka kwa jina la Yesu Kristo kwenda
kwenye maneno Baba mwana na Roho mtakatifu na kanisa Katoliki katika karne ya
pili”(Catholic Encyclopedia
book II p. 263)
Ni kanisa katoliki ndilo lililo badili mstari huu wa biblia ili kuingiza
mstari ambao uonekane kuwa unathibitisha kuwepo kwa utatu mtakatifu. Lakini
japokuwa wametumia njia hii ya udanganyifu, lakini bado mstari huu
hauthibitishi kuwepo kwa Mungu mwenye nafsi tatu. Katika maandiko ya kale ya
Eusebius anasema
“Katika neno moja na sauti alisema Nendeni na mfanye mataifa wanafunzi
wangu kwa Jina langu wafundishe kuyashika yote niliyo waamuru” (Proof of the Gospel by Eusebius book III ch 6, 132 (a)
p. 152)
Eusebius alikuwa ni mwana historia wa kikatoliki katika karne ya pili na ya
tatu pia alikuwa ni Askofu wa Kaesaria.
Katika kitabu chake ananukuu mstari wa Mathayo 28:19 kutoka katika maandiko ya
Kitabu cha mathayo halisi ambayo yaliandikwa kwa wino wake Mathayo. Katika
Nukuu hiyo inaonesha jinsi gani ilivyo tofauti kabisa na jinsi Mstari huu
unavyosomeka leo hii. Kanisa Katoliki lilibadili mstari huu ili kuufanya
uonekane kuwa unaunga mkono uwepo wa nafsi tatu za Mungu. Yoyote asomaye huu
mstari anatambua kuwa ni mstari ambao unapingana na mistari mingine ya Biblia
ambayo imesema wazi kuwa Ubatizo ni kwa jina la Yesu na sio Jina la Baba mwana
na Roho mtakatifu. Maneno haya Kwajina la Baba na la Mwana na la Roho mtakatifu
ni neno linalotumiwa sana na kanisa katoliki katika sala. Kwa nini wanatumia
sana haya maneno? Ni kwasababu kanisa lenyewe ndilo limeyaongeza maneno haya
katika Biblia. Katekisim ya kanisa katoliki inasema
“Biblia inatuambia kuwa wakristo walibatizwa ndani ya Kristo (no.6). Ni
mali ya Kristo. Matendo ya Mitume (2:38,8:16,10:48,19:5) inatuambia kuhusu
kubatiza kwa jina la Yesu. Tafsiri nzuri ingekuwa ndani ya jina la Kristo. Ni
katika karne ya nne tu kanuni ya Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho
mtakatifu ikawa ni desturi”
(Bible Catechism Rev, John C Kersten, S.V.D.., Catholic Book Publishing co, N.Y
1973 p. 164)
Katekism ya Kanisa Katoliki inatuambia kuwa ni karne ya nne kanuni ya
kubatiza kwa jina la Baba na la Mwana na La Roho mtakatifu ikawa ni desturi.
Inamaana kuwa yapokuwa badiliko la mstari wa Mathayo 28:19 lilifanyika katika
karne ya pili lakini haikuwa ni desturi mpaka kufikia karne ya nne ndio ikawa
ni desturi kubatiza kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho mtakatifu. Ni wazi
kuwa ilichukua muda sana mpaka jambo hili kukubalika maana mitume walibatiza
kwa jina la Kristo wala sio kwa jina la Baba na la mwana na la Roho mtakatifu.
Kardinali Rotzinger anasemaje
Msingi wa Msimamo wetu wa (Mathayo 28:19 utatu) wa Imani, ilichukua umbile katika kipindi cha karne ya pili na ya tatu kwa kushirikiana na sherehe ya ubatizo. Katika kuangalia asili, Maneno haya (Mathayo 28:19) yalitoka katika jiji la Roma” (Joseph Ratzinger-Pope Benedict XVI, Introduction to christianity 1968 p 82, 83)
Msingi wa Msimamo wetu wa (Mathayo 28:19 utatu) wa Imani, ilichukua umbile katika kipindi cha karne ya pili na ya tatu kwa kushirikiana na sherehe ya ubatizo. Katika kuangalia asili, Maneno haya (Mathayo 28:19) yalitoka katika jiji la Roma” (Joseph Ratzinger-Pope Benedict XVI, Introduction to christianity 1968 p 82, 83)
Kardinali Joseph Ratzinger ambaye baadaye akaja kuwa Papa Benedict XVI anasema
wazi kuwa maneno yaliyopo katika Mathayo 28:19 yalitoka katika jiji la Roma
katika kipindi cha Karne ya pili na ya tatu. Kanisa Katoliki lenyewe linakiri
kuwa maneno kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho mtakatifu yaliongezwa
katika biblia na kanisa katoliki huko Roma. Maneno haya hayakuwepo kabisa
katika Kitabu halisi cha Mathayo. Mwana historia Edmund Schlink anasema
“Amri ya ubatizo katika Mathayo 28:19 haiwezi kuwa ni historia halisi ya
ubatizo wa Kikristo. Ni lazima angalau kuwa maneno haya yamebadilishwa katika
umbo na kuongezwa na Kanisa katoliki” (Edmund Schlink The doctrine of Baptism p. 28,1972)
Mpaka kufikia hapa tumeweza kuelewa kwanini Mistari wa Mathayo 28:19 ni
tofauti na mistari mingine inayohusiana na Ubatizo. Tumeweza kujifunza kuwa
Biblia inatambua ubatizo kwa jina la Yesu Kristo na sio Kwa jina la Baba na la
Mwana na la Roho mtakatifu. Kwa kweli Mungu hata siku moja hawezi kutuacha
gizani bali anatoa ukweli ili tuweze tukawa huru. Kila msomaji na afahamu kuwa
fundisho la utatu mtakatifu halina msingi wowote katika maandiko matakatifu wala
hakuna sehemu yoyote ile ambayo utaona kuwa imeandikwa kuwa “Mungu ni nafsi
tatu”. Wala hakuna sehemu hata moja ambayo utaona inasema Baba mwana na Roho ni
nafsi tatu za Mungu. Wakati umefika kumwabudu Mungu anayefunuliwa ndani ya
Biblia na sio Mungu aliyetengenezwa na Kanisa Katoliki. Watu wa Mungu
wanamtambua Mungu aliyezifanya Mbingu na nchi na Kumwabudu Mungu aliye
Mbinguni.