MUNGU ANA NAFSI NGAPI?
Ni wazi kuwa kila mmoja katika kanisa la Adventista wasabato na
Wale ambao sio wasabato watajibu swali hili kuwa Mungu ana nafsi Tatu. Hii ni
kutokana na Fundisho la Utatu mtakatifu. Nianze kwa eleza nini maana ya
fundisho la utatu mtakatifu, Hili ni fundisho linalosema Mungu ni nafsi tatu
yani Baba, mwana na Roho mtakatifu. Kwa maana nyingine ni kwamba Mungu hawezi kuwa na nafsi moja bali
siku zote ni tatu. Lakini Swali la
kujiuliza ni kwamba Je biblia Takatifu imesema Mungu ana nafsi tatu? Au ni
mapokeo Kutoka katika kanisa Katoliki. Mwanafunzi yoyote mwenye nia ya kweli ya
kujifunza pima hichi ninachokisema kama kimetokana na Biblia au hapana, kwa
kutambua hilo basi inabidi tuangalie biblia kama jinsi inavyojifunua Yenyewe.
Ni muda umefika ambapo inabidi tumwabudu Mungu aliyefunuliwa katika Biblia na
sio Mungu aliyetengenezwa na kanisa Katoliki, muda umefika ambapo kanisa la
wasabato linabidi liamshwe ili kuzingatia ujumbe wa malaika wa kwanza, ujumbe
ambao kanisa la Mungu limeuweka pembeni au wenda hawajui unahusiana na nini.
Lakini jambo moja tu ambalo ni wazi ni kwamba Mungu wa Mbinguni kwa kupitia
maandiko yake huwa anajitetea na kujidhihirisha kuwa yeye ndiye Mungu wa
Biblia. Tufunue Biblia Zetu tuangalie Biblia yenyewe inasemaje.
"Mkumbuke Ibrahimu na isaka na Israel watumishi wako ambao Uliwaapia
KWA NAFSI YAKO na kuwaambia Nitazidisha kizazi chenu mfano wa nyota za
mbinguni. Tena nchi hii yote niliyoinena nitakipa kizazi chenu nao watairithi
milele"
(Kutoka 32:13).
Tukisema Mungu ana nafsi tatu tunapingana na Mstari huu unaoonesha wazi kuwa
Mungu ana nafsi moja. Nafikiri kwa sisi tunaotumia kiswahili pale tunapotumia
neno “kwa nafsi yako” kitu gani kinakuja akilini? Kwamba nafsi ni moja au
zaidi ya moja? Ni wazi kuwa mstari umeonesha kuna nafsi moja. Tuone pia mstari
mwingine unasemaje.
“akasema Nimeapa KWA NAFSI YANGU asema BWANA kwa kuwa umetenda neno hili
wala hukunizuilia mwanao mwanao wa pekee. Katika kubariki nitakubariki na
katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni na kama mchanga
ulioko pwani na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao"( Mwanzo 22: 13).
Ikiwa Tunafikiri kuwa Mungu ana nafsi tatu tujue kuwa Sio Mungu wa Biblia
na sio jinsi Mungu anavyojifunua Yeye
mwenyewe maana katika mstari huu Mungu amesema wazi “kwa nafsi yangu” si dhani
kuwa kuna mtu yoyote anayeweza tumia neno kwa nafsi yangu akimaanisha nafsi
tatu. Maana kama ingekuwa ni tatu basi ingekuwa ni nafsi zetu. Kama Mungu
angekuwa ni zaidi ya nafsi moja basi wingi ungetumika kuwa ameapa kwa nafsi
zake. Lakini Mungu hasemi hilo, sasa sisi tunapata wapi hili jambo? Tuangalie
mstari mwingine unasemaje.
"Bwana MUNGU ameapa KWA NAFSI YAKE asema BWANA Mungu wa majeshi
Naizira Fahari ya yakobo, nachukizwa na majumba yake kwasababu hiyo nitautoa
huo mji pamoja na wote waliomo ndani yake" (Amosi 6:8)
Hakika Mungu ni Mungu mwenye nafsi Moja. Katika yeye katika hakuna nafsi
nyingine. Maana kama kungekuwa na zaidi ya nafsi moja angesema wazi kabisa.
Lakini Mungu wetu ni Mungu anayependa kutufunulia ukweli wa biblia ili tupate
kuwa huru. Mungu ameapa kwa nafsi yake, maana yake ni Kwamba yeye ni nafsi moja
kama jinsi tulivyo mimi na wewe. Kama sisi tu nafsi moja, hata Mungu wetu naye
ni hivyo hivyo maana tumeumbwa kwa mfano na sura yake. Tuendelee kuangalia
Biblia inasemaje.
"BWANA wa majeshi ameapa KWA NAFSI YAKE akisema Hakika Nitakujaza watu
kama Nzige nao watapiga kelele juu yako" (Yeremia 51: 14)
Ni wazi kuwa Mungu wa mbinguni ni Mungu mwenye nafsi Moja. Kwanini katika
biblia kuwe na marudio ya neno moja tu kuwa ameapa kwa “nafsi yake” kama Mungu
angekuwa ni nafsi tatu? Au je walioandika biblia walikosea katika uandishi wao?
Hapana Bali yote yaliyoandikwa katika biblia ni pumzi ya Mungu. Ni Mungu
mwenyewe anajidhihilisha wazi kuwa yeye ni mmoja tu. Mungu anashuhudia kuwa
yeye ni nafsi moja kama jinsi mimi na wewe tulivyo na nafsi moja tu. Mungu
anarudia mara kwa mara akionesha kuwa yeye ni nafsi moja tu wala hakuna
mwingine.
"Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye mteule wangu, ambaye NAFSI YANGU
imependezwa Naye nimetia roho YANGU juu yake naye atawatolea mataifa hukumu"(Isaya 42:1)
Mungu anaendelea kusisitiza kuwa ni nafsi moja tuu na sio tatu kama jinsi
tulivyofundishwa. Katika hili ninaujasiri wa kusema hilo. Kwasababu Mungu
mwenyewe anashuhudia hilo. Kama tuliweka mbali ushabiki wa kidini na
wakimafundisho na kuanza kutazama vyema maandiko matakatifu utaona jinsi gani
Mungu mwenyewe anajionesha kwetu. Kama Mungu angekuwa na nafsi zaidi ya moja
basi asingesema kuwa nimeapa “kwa nafsi yangu”.
Tunaposema neno “Yangu” Je huwa tunamaanisha nafsi zaidi ya moja? Hapana
lakini cha kushangaza ni kwamba tunapokuja kwa upande wa Mungu basi akili zetu
zinapumbazwa na fundisho ambalo halipo katika biblia. Tuendelee kuangalia
MIMI BWANA nimekuita katika haki nami nitakushika mkono na kukulinda
na kukutoa uwe agano la watu na nuru ya mataifa"( Isaya 42: 6)
Sidhani mpaka Mungu aseme neno “Mimi” bado tu amaanishe nafsi zipo tatu.
Ndugu zangu katika Bwana tuache biblia ijitetee, tuache biblia ijitafsiri.
Tuchunguze kile tunachofundishwa kanisani kama kweli kimetokana na Biblia.
Tuache Mungu mwenyewe aseme kuwa yeye ni nafsi moja au tatu. Ndugu zangu
tusifanye mioyo yetu kuwa migumu kiasi cha kubishia mpaka Mungu mwenyewe aliyejifunua
kwetu sisi. Je Kuna Mungu mwingine? Tuone jinsi gani Mungu wetu anachosema
"Fahamu sasa ya kuwa MIMI naam MIMI NDIYE wala hapana MUNGU MWINGINE
ila MIMI. Naua MIMI, nahuisha MIMI. Nimejeruhi tena naponya wala hapana awezaye
kuokoa katika mkono WANGU.
( Kumb 32: 39)
Wewe msomaji ni shahidi jinsi Mungu anavyojifunua. Unaona wazi jinsi gani
neno lake ni lipo wazi kuwa yeye Mungu ni nafsi moja tu. Kama Mungu angekuwa
zaidi ya nafsi moja, sasa kwanini aseme neno “Mimi” badala ya “sisi”. Hili tu
liache likikuumiza akili kufikiria. Hili tu likufanye utafakari kile ulichokuwa
unakijua kuhusu Mungu. Kwani je Neno linalotoka kwa Mungu si neno la kweli? Au
je kuna kosa gani lililopo katika Biblia takatifu ya Mungu? Sasa kama hakuna
kosa lolote kwanini tunaendelea kuamini kuwa Mungu ni nafsi tatu wakati Mungu
mwenyewe amesema wazi kuwa yeye ni nafsi moja tu? Bila Shaka hakuna Mungu
mwingine ila yeye. Mungu mmoja mwenye nafsi moja.
"MIMI NI BWANA wala Hapana mwingine zaidi yangu MIMI hapana Mungu,
nitakufunga mshipi ijapokuwa hukunijua"( Isaya 45: 5)
Tazama jinsi Mungu anavyorudia kuelezea. Tazama Mungu ambavyo hachoki
kusisitiza kuwa yeye ni mmoja tu na sio watatu. Tazama Jinsi Mungu
anavyoendelea kutoa maelezo kuwa bila yeye hakuna mwingine. Kwa jinsi gani
Mungu anatupenda kiasi cha kwamba hataki atuache gizani katika mafundisho la uongo kutoka kanisa katoliki. Eeh Mungu endelea Kuzungumza na wale
wanaosema wewe ni Nafsi tatu.
Lakini MIMI NI BWANA Mungu wako tangu nchi ya Misri wala hutamjua
mungu mwingine ila MIMI wala zaidi ya MIMI hakuna mwokozi" (Hosea 13: 4)
Mungu mwenye nafsi moja huyo ndiye Mungu wa kweli. Yoyote anayesoma Neno la
Mungu katika uaminifu wa Moyo ataweza kugundua kuwa Biblia huwa haijipingi.
Biblia imesema wazi kuwa Mungu wetu Mungu wa mbingu na nchi ni Mungu mmoja
mwenye nafsi moja tu. Kama angekuwa ni zaidi ya moja basi Mungu wetu angetueleza
wazi. Lakini katika maandiko yake matakatifu Mungu amejifunua kwetu ili tupate
kuwa huru kutoka katika mafundisho yanayo mvunjia heshima maana hakuna mnyama
wala binadamu aliye na nafsi tatu.
"Bali BWANA ndiye Mungu wa Kweli. Ndiye Mungu aliye hai, Mfalme wa
milele, Mbele za ghadhabu YAKE nchi yatetemeka. Wala mataifa hawawezi
kustahimili hasira YAKE"
( Yeremia 10:10)
Baada ya kuona Jinsi biblia inavyojieleza na kujibu swali Kwamba Mungu ni
mwenye Nafsi Moja na Biblia inamtaja Kuwa ni Mungu pekee tuangalie katika
Vitabu vya agano jipya Vinasemaje. Je Mungu aliyefunuliwa katika vitabu
vinavyojulikana kama vitabu vya agano la kale ni tofauti na Mungu aliye katika
vitabu vya agano jipya. Au je Mungu katika agano jipya ni Mungu mwenye nafsi
tatu lakini katika agano la kale ni Mungu mwenye nafsi moja? Ili tupate majibu
ya maswali yetu tuendelee kuangalia nini ambacho biblia inasema.
"Twamshukuru Mungu, Baba yake Bwana wetu Yesu Kristo siku zote
tukiwaombea"(wakolosai
1:3)
Mtume paulo anasema wazi kuwa Mungu ni mmoja ambaye ndiye Baba wa bwana
wetu Yesu Kristo. Nafikiri hakuna mstari katika biblia ulio wazi kama huu.
Mstari umeweka bayana kuwa Mungu ni baba yake Yesu Kristo. Yesu ana baba mmoja
tu, na huyo baba ndiye Mungu. Yule Mungu aliyeapa kwa nafsi yake katika agano
la kale. Ndiye yule Mungu aliyesema hakuna “Mungu mwingine ila mimi” katika
agano la kale.
"Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo aliyetubariki kwa
baraka zote za rohoni katika ulimwengu
wa roho ndani yake Kristo"( Waefeso 1: 3)
Mtume Paulo anaendelea sisitiza
kwako kuwa Mungu si nafsi tatu Kuwa Mungu ni mmoja aliye baba wa Bwana
Yesu. Baba ni mmoja hivyo Mungu ni mmoja. Hakuna neno wazi kama hili. Mungu
amejidhihilisha mara nyingi akishuhudia kuwa yeye ni nafsi moja tu. Mtume Paulo
hakufundisha kuwa Mungu ni zaidi ya nafsi moja. Bali alisema wazi kuwa Mungu ni
mmoja aliye baba wa Mwana wa Mungu Yesu Kristo.
"Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa Rehema,
Mungu wa faraja yote"(2wakoritho
1:3)
Mtume Paulo anaendelea tukoa msisitizo kwako kuwa Mungu ni
nafsi tatu kwamba sio hivyo ila Mungu ni nafsi moja Naye ndiye Baba wa wa Bwana
wetu Yesu Kristo. Mungu wetu huwezi nyamaza kimya kama kuna uongo unaoonekana
kulibeba kanisa. Paulo ameweka bayana kuwa Baba pekee ndiye Mungu mmoja zaidi
ya hapo Paulo mtume wa Mungu hakusema chochote.
Lakini kwetu sisi MUNGU NI MMOJA TU, ALIYE BABA ambaye vitu vyote
vimetoka kwake nasi tunaishi kwake, yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo ambaye
kwake vitu vyote vimekuwapo na sisi kwa yeye huyo"(1 Wakorintho 8:6)
Msomaji ni shahidi kuwa mstari huu umejikamilisha. Na kubaliana sawa sawa
na kile kilichoelezwa katika agano la kale. Hakuna ukweli kama huu ya kuwa
Mungu ni Baba, na Baba ndiye Mungu. Yeye ndiye aliyesema hakuna mwingine ila
yeye. Yesu Naye anasema Hili.
"Yesu akamwambia usinishike kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba, Lakini
enenda kwa Ndugu zangu ukawaambie Ninapaa Kwenda kwa BABA YANGU NAYE NI BABA
YENU, KWA MUNGU WANGU NAYE NI MUNGU WENU" (Yohana 20:17).
Yesu anaweka wazi kuwa Baba yake ndiye Mungu wetu Baba Mmoja mwenye nafsi
moja ndiye Mungu wetu, Yesu anaongea na
wewe Kuwa yeye daima ni Nafsi moja tu. Yesu naye ana Mungu wake ambaye ndiye
Baba. Yesu amesema wazi kuwa baba yake ndiye Mungu wa mbingu na nchi.
"Na uzima wa Milele ndio huu wakujue wewe MUNGU WA PEKEE WA KWELI na Yesu kristo uliyemtuma" (Yohana 17:3)
Mjue
Mungu wa kweli upate uzima wa milele, usifanye moyo wako kuwa mgumu, mwabudu
Mungu mwenye nafsi moja ambaye ni Baba, tambua kuanzia sasa kwamba Kuna Baba
mmoja huyo Baba ndiye Mungu wa kweli. Wakati umefika tumwabudu Mungu aliye
kwenye Biblia na sio Mungu wa kutengenezwa na Mistari michache ya Biblia
iliyotafsiriwa vibaya tuangalie na kuijadili Mistari hii michache iliyopotoshwa
ili kuonekana kuwa ina thibitisha utatu katika sura ifuatayo. Tumwabudu Baba
yeye ndiye Mungu wa Kweli ndani yake hakuna Nafsi nyingine ila Yeye pekee yake. Wenda msomaji anaweza kujiuliza vipi kuhusu ule mstari unaosema wapo watatu washuhudiao mbinguni Baba neno na Roho na hawa ni umoja (1yohana 5:8) na ule wa Kwa jina la Baba na mwana na Roho mtakatifu (Mathayo 28:19). usikose kusoma post inayofata imeeleza wazi kabisa kuhusu mistari hii ambayo kwa mara nyingi huwa inatumika kufundisha kuwa Mungu ni utatu.