ASILI YA FUNDISHO LA UTATU.


Katika Historia ya ulimwengu fundisho la utatu lilikuwa sio fundisho geni masikioni pa watu. Jamii ya kale ya kigiriki na wamisri na dunia nzima walikuwa na imani ya utatu. Sasa Nianze kwa kutoka nukuu mbali mbali kutoka katika vyanzo vya historia vinavyoheshimika Duniani. Encarta Encyclopedia inasema

"Fundisho la Utatu katika teolojia ya kikristo ni fundisho linalosema kuwa Mungu yupo katika nafsi tatu ambazo ni  Baba, Mwana na Roho mtakatifu ambapo nafsi hizi zimeungana na kuwa kitu kimoja. Fundisho hili halifundishwi katika Vitabu vya Agano Jipya ambapo Neno "Mungu" mara zote linamlenga Baba". (Encarta Encyclopedia)

Kila mmoja ni shahidi kuwa Vitabu vya agano jipya Mara zote huwa vinamtaja Baba pekee kuwa yeye ndiye Mungu Msomaji anaweza kujiuliza vipi kuhusu 1yohana 5:8 na Mathayo 28:19, Post hii haitozungumzia ila usikose kusoma Post inayofata lakini msomaji akisoma mistari hio hawezi kuona sehemu inayosema Mungu ni nafsi tatu. 

"Lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake nasi tunaishi kwake yuko na Bwana mmoja Yesu kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo na sisi kwa yeye huyo"( 1wakorintho 8:6)

Paulo anasema Wazi kuwa Baba ndiye huyo Mungu mmoja mwenye nafsi moja. Lakini  Fundisho la utatu linakataa na kusema Baba sio Mungu mmoja pekee, bali yeye ni miongoni mwa wengine wawili wanashirikiana kuunda Mungu mmoja. Kitu ambacho Biblia inakataaa wazi na kusema Baba pekee ndiye Mungu mmoja tu, wala Biblia haisemi kuwa Baba Mwana na Roho ni nafsi tatu za Mungu. Tunajua kuwa Mungu ni nafsi moja kutokana na ushahidi anaojishuhudia yeye mwenyewe.
"Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye mteule wangu, ambaye NAFSI YANGU imependezwa Naye nimetia roho YANGU juu yake naye atawatolea mataifa hukumu"(Isaya 42:1)
“akasema Nimeapa KWA NAFSI YANGU asema BWANA kwa kuwa umetenda neno hili wala hukunizuilia mwanao mwanao wa pekee. Katika kubariki nitakubariki na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni na kama mchanga ulioko pwani na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao"( Mwanzo 22: 13).

Kwa kusema nafsi yangu tunajua kuwa Mungu ni nafsi moja si zaidi ya hapo. Tukumbuke kuwa Encarta Encyclopedia sio kitabu cha dini bali ni kitabu cha Historia.Tuangalie Mwana historia Edward Gibbons anasema
"Kama upagani ulishindwa na ukristo ni kweli kwa upande mwingine kuwa Ukristo ulipotoshwa na upagani. Imani ya kweli ya wakristo wa kwanza ilibadilishwa kwa kupitia kanisa la Roma kuwa Imani isiyoeleweka hasa Fundisho la utatu. Mafundisho mengi ya upagani kutoka Misri na kuungwa mkono na Plato yalibaki kama ni mafundisho muhimu ya Imani"(Edward Gibbons, History of Christianity, 1916)

Mwana historia huyu anasema wazi kuwa Fundisho la utatu asili yake ni upagani na moja ya chanzo ilikuwa ni ushawishi wa  mwanafalsafa wa kipagani aliyekuwa anaitwa Plato. Plato katika Falsafa zake alisema Kuwa uungu ni nafsi tatu zinazoungana na kuwa Kitu kimoja. Au kwa tafsiri nyingine Nafsi tatu za uungu zinaungana na kuunda Mungu mmoja. Falsafa yake ilienea sana katika Ulimwengu wa kipagani duniani na Dini mbali mbali za kipagani zikawa na Utatu wa miungu unaounda Mungu mmoja. Wa misri walikuwa utatu wa Osiris, Horus na Seth. Mwanahistoria Edward Gibbons anasema kuwa Kama ukristo uliwahi kushindwa na upagani, basi ni wazi kuwa upagani ulichafua imani ya kweli ya biblia na kuleta imani isiyoeleweka hasa fundisho la utatu. Kwanini mwandishi huyu wa historia aseme jambo kama hili? Ni kwasababu Fundisho la utatu lilikuwepo hata kabla ya ukristo. Plato aliishi kipindi ambacho ni kabla ya kuzaliwa Kwa Yesu Kristo, na katika kipindi hicho fundisho la utatu lilikuwepo na Plato alifundisha kitu ambacho kilikuwepo hata kabla yake. Mwana historia huyu anasema kuwa Mafundisho ya mwanafalsafa wa kipagani Plato ndio baadaye yanakuja kuwa ni  mafundisho muhimu katika imani ya kikristo. Kila mmoja ambaye anajua jinsi ibada ya jua ilivyoingizwa katika ibada ya kikristo lakini chimbuko lake sio katika maandiko ya biblia, ni sawa kabisa na jinsi fundisho la utatu lilivyoingia katika ukristo wakati chimbuko lake likiwa nje  maandiko matakatifu ya biblia. Mwana historia Siefried Morenz anasema

"Utatu ulikuwa ni fundisho kuu katika teolojia ya wamisri. Miungu mitatu iliyoungana na kuheshimiwa kama mungu mmoja, na kujulikana katika umoja. Kupitia hili ushawishi mkubwa wa kiroho kutoka dini za Kimisri iliionesha kuhusika katika Teolojia ya Kikristo."(Siegfried Morenz, Egyptian Religion, 1960)

Mwanahistoria Huyu anasema wazi kuwa dini za wamisri zilikuwa zinafundisha sana Utatu wa miungu na kupewa heshima na kuabudiwa kama hawa watatu ni mungu mmoja. Pia anasema wazi kuwa fundisho hili kutoka dini ya upagani za Misri imechangia katika kuanzisha fundisho la utatu katika teolojia ya kikristo. Mwanahistoria Siefried Morenz anafafanua vizuri kile ambacho tumeona katika maandiko ya kihistoria yaliyoandika na Edward Gibbons, Morenz anaweka wazi kuwa fundisho la utatu lilikuwepo katika enzi za wamisri, yani kipindi hata kabla ya kuwepo kwa Ukristo. Wamisri walikuwa wanaamini kuwa miungu mitatu inaungana na kuheshimiwa kama ni mungu mmoja. Hii ndio ilikuwa ni teolojia au imani ya wamisri katika imani yao ya kipagani ya kale, mwandishi anasema wazi kuwa Imani hii baadaye ilikuja kuwa tena ni imani ya kikristo sawa na kile ambacho Edward Gibbons alisema. Mpaka hapa tunagundua kuwa Imani ya utatu ilikuwepo hata kabla ya kuwepo kwa ukristo, pia tunajifunza kuwa Imani hii asili yake ni Misri na baadaye ikaenea maeneo mbali mbali ya ulimwengu.
Katika Dini ya kihindu walikuwa na utatu wa Siva, Brahma na Vishnu. Mwandishi mmoja anasema

"Hawa watatu (Brahma, Vishnu na Siva) wamechangia kuwepo kwa utatu wa kihindu (Trimurti, Mmoja katika asili tatu).Uelewa huu ulijaribu kutengeneza na kuweka usawa kwamba nguvu ya Uungu ni moja inayochangiwa na miungu mbali mbali katika shughuli za kila siku za ibada" (A. Parthasarathy, symbolism of Hindu gods and rituals, 1989)


Hii ni picha ya Utatu wa kihindu. Katika upande wa Asia tunaona kuna imani ya utatu. Wahindu walikuwa na  utatu katika dini yao ya kihindu. Kuwa hawa watatu walikuwa wanapewa heshima kama vile ni mungu mmoja. Mpaka leo dini ya kihindu inamiungu wengi sana lakini wote wanaamini japokuwa miungu ni wengi ilawote wanapata nguvu moja ya uungu kutoka katika utatu wa  Siva, Vishnu na Brahma. Kila mmoja ambaye ni mwanafunzi wa mzuri wa biblia anatambua kuwa kama jinsi Ibada ya jua katika siku ya jua ilivyoingia katika ukristo kwa kupitia kanisa katoliki (Sunday) ndivyo ilivyo katika fundisho la utatu. Kama jinsi Ibada ya jumapili ilivyotafutiwa mistari katika biblia iliionekane kuwa Jumapili ipo katika maandiko matakatifu ndio sawa na fundisho la utatu. Mwana historia Alexander Hislop anasema

"Upapa katika makanisa yake baadhi  kwa mfano wanaojulikana kama wanautatu wa Madrid wana picha inayoonesha mungu watatu walioungana, wenye vichwa vitatu katika mwili mmoja. Wababeli walikuwa na kitu kama hicho pia. Layard katika kazi yake ya mwisho alionesha vielelezo kuhusu mungu watatu walioungana waliokuwa wanaabudiwa huko assyria ya kale ikienda sambamba na ibada za kishetani za miungu inayofanana na hiyo iliyokuwa inaabudiwa na  wapagani wa siberia..Huko India vile vile katika moja ya mahekalu yaliyo katika mapango ya kale yalikuwa yamechorwa vichwa vitatu katika mwili mmoja katika jina la Eko, deva  trimurti yani mungu mmoja katika asili tatu. Huko Japani ibada ya kibuddha ilikuwa na mungu buddha aliyekuwa na vichwa vitatu katika mwili mmoja aliyekuwa anajulikana kama  "San pao Fuh". Haya yote yalikuwepo katika ulimwengu wa kale uliokuwa umejawa na ibada za Sanamu. utatu ulijulikana Ulimwenguni pote katika nchi zote za kale za ulimwengu."( Alexander Hislop The two babylon pg 17-18, 1853)

Picha hizi  ni Picha zinazoonesha utatu wa miungu. Upande wa Kushoto ni picha ambayo ilikuwepo katika makanisa ya kikatoliki inayoonesha kuwa Mungu wa kikristo ni utatu. Upande wa Kulia ni Picha ya Buddha ambaye pia wanaamini naye ni utatu. Tunaona kuwa kuna ufanano mkubwa sana kati ya mungu aliye ndani ya kanisa katoliki na mungu wa kibuddha. Tukumbuke kuwa Dini hii ya buddha ilikuwa ni dini ya kale kuliko Ukristo. Fundisho la utatu lilikuwa ni fundisho la zamani sana kabla hata kuwepo kwa dini ya kikristo. Mwana historia  Alexander Hislop ameweka wazi kuwa utatu ulikuwa ni imani katika dini nyingi sana za upagani, Anaeleza kuwa wabuddha walikuwa na buddha aliyeungana vichwa vitatu katika mwili mmoja, na kitu hicho hicho anakiona pia katika Makanisa ya kikatoliki hasa kule madrid. Mpaka hapa tunaona kuwa wanahistoria hawa wanaeleza wazi kuhusu asili ya fundisho la utatu. Wanahistoria hawa wote tuliowaona mpaka sasa wanatosha kukuletea picha halisi ya asili ya fundisho la utatu. Lakini tunaendelea mbele kuangalia vitabu vya historia vinatuambia nini kuhusu fundisho la utatu. Encyclopedia Britannica inasema,

"Fundisho hili lilianza taratibu katika kipindi cha karne nyingi kwa kupitia mabishano mengi" (Encyclopedia Britannica, article Trinity).
Kanisa Katoliki mwaka 325AD ndio waliingiza fundisho hili la kipagani katika imani ya kikristo fundisho la utatu linaingia kanisani zaidi ya miaka 300 tokea biblia iandikwe. Ili ionekane kuwa ni fundisho la Biblia kanisa katoliki lilisingizia na kuongeza baadhi ya mistari katika biblia iliionekane kuwa Mungu ananafsi tatu. Encyclopedia Inasema kuwa fundisho hili liliingia taratibu maana yake ni kwamba ilichukua muda sana kukubalika na lilisababisha mabishano mengi sana. Mabishano hayo ni mabishano kati ya maaskofu wa kanisa katoliki. Lakini kanisa katoliki lenyewe linakubali kuwa fundisho hili ni lao na halikutoka katika Biblia takatifu. Na hii ni kebehi kubwa sana kwa wanaojiita waprotenstanti ikiwapo kanisa la waadventista wasabato. Jarida la kikatoliki la Life magazine linasema

"Wapinzani wetu mara nyingine wanadai kuwa fundisho lolote ambalo halipo katika maandiko halitakiwi kushikiliwa. Lakini makanisa ya kiprotestant yenyewe yamekubali mafundisho hayo kama vile utatu ambalo halina msingi wowote katika injili"( Assumptions  of Mary, Life magazine october 30, 1950)

Kanisa katoliki linajua kuwa hili fundisho halipo katika Biblia. Linajua hakuna sehemu katika biblia inayosema Mungu ni nafsi tatu wala hakuna sehemu inathibitisha Baba, mwana na Roho ni nafsi tatu za Mungu. Kanisa katoliki linawashangaaa waprotestanti wanalitetea fundisho hili kwa kutumia maandiko ambayo hayana uhusiano wowote na kuwepo kwa nafsi tatu za Mungu. Kanisa katoliki linasema wazi kuwa fundisho hilo halina msingi wowote katika maandiko matakatifu, na ndio kanisa ambalo hili fundisho limetokea. Kwa kutetea fundisho la utatu ni kutetea mamlaka ya papa.  Kanisa katoliki linajua wazi kile ilichokifanya katika historia. New universal Dictionary inasema
"Utatu wa kiplato wenyewe ni utatu uliotoka katika mafundisho ya utatu ya zamani na kurudi nyuma kwa watu wa zamani..falsafa ya utatu ndio imesababisha kuzaliwa kwa nafsi tatu za Mungu zinazofundishwa leo na wakristo. Fundisho hili la huyu mwanafalsafa la utatu linaweza kuonekana katika dini zote za kale za kipagani"(new Universal dictionary)

New Universal dictionary ni kitabu kinachoandikwa kwa lugha ya kifaransa. Kinasema kuwa Utatu uliokuwa unafundishwa na Plato ulikuwa ni utatu ambao asili yake ilikuwa ni utatu wa zamani. Maana yake ni kwamba hata Plato alikuwa anafundisha utatu alioukuta, alikuwa anafundisha utatu ambapo ulikuwepo hapo kabla hata kabla yake. Mwandishi anasema kuwa utatu uliokuwa unafundishwa na plato ndio ulipelekea kuwepo kwa fundisho la kuwepo kwa nafsi tatu za Mungu kama hivi leo linavyofundishwa katika makanisa ya Kikristo. Katika kitabu cha the church in the First three centrury mwandishi anasema

"Fundisho la Utatu liliundwa taratibu na lilichelewa sana kuundwa. Chanzo chake ikiwa ni kigeni kutoka kwa Wayahudi na maandiko ya kikristo. Fundisho hili limesitawi na kuingia katika ukristo kwa kupitia mababa waliokuwa wafuasi wa Plato.(Alvan Lamson, The church in the first three Century,1860)
Mpaka kufikia hapa tunaona kuwa Utatu unaofundihswa katika makanisa ya kikristo ni utatu ambao ulikuwa unafundishwa na Plato kipindi cha zamani. Wana historia wanaendelea kutoa ushahidi kuwa utatu hauna misingi yoyote katika maandiko bali misingi yake ilikuwa ni misingi ya kigeni nje ya Uyahudi ambao ndio chimbuko la dini ya kikristo. Ukristo ulitokea katika dini ya kiyahudi. Yesu alikuwa ni myahudi na aliishi maisha ya kiyahudi, alichofundisha hasa ni kwamba wayahudi wamtambue kuwa yeye ndiye masihi aliyetabiriwa kuwa atakuja kwao. Lakini Wayahudi wao wanaamini katika Mungu mmoja tu. Na Yesu alifundisha kuwa Kuna Mungu mmoja tu ambaye ndiye Baba yake wa pekee. Alifundisha wazi kuwa yapokuwa yeye amerithi asili ya Baba yake ya uungu lakini yeye sio Mungu katika cheo bali Baba yake. Lakini miaka zaidi ya 300 tokea Yesu arudi kwa Baba, kanisa sasa linakuja na fundisho kuwa Mungu sio tena mmoja bali Mungu ni watatu. Kitu ambacho hakikuwepo kabisa katika Imani ya kiyahudi, kitu ambacho Yesu hakuwahi kufundisha, kitu ambacho hata mitume hawakuwahi kufundisha. Maana yake ni kwamba chanzo hiki hakitokani na maandiko au imani ya kiyahudi bali inatoka katika chanzo ambacho ni kigeni na hakihusiani kabisa na Imani ya kiyahudi ambayo ilikuwa imejengwa na Mungu mwenyewe alipowatoa wana wa Israel kutoka katika mateso ya wamisri. Tuendelee kuangalia ushahidi wa kihistoria kuangalia asili ya hili fundisho la utatu. New Bible dictionary inasema,

Neno utatu halipatikani katika Biblia..Halikupata nafasi yoyote rasmi katika teolojia ya kanisa mpaka karne ya nne...sio fundisho la biblia katika mantiki kwamba kila hatua ya kuanzishwa kwake inaweza kuonekana katika Biblia..Maandiko matakatifu hayatupi chimbuko la kuanzishwa kwa fundisho la utatu. (New Bible Dictionary, 1982).

Tunaona kuwa Mungu anasema wazi kuwa yeye ni nafsi moja tu na hakuna nafsi nyingine ambayo inafaa kuitwa Mungu bali ni Yeye pekee. Vitabu vya agano la kale na vile vya agano jipya vyote kwa pamoja vimesema kuwa kuna Mungu mmoja ambaye ndiye Baba wa Mwana wa Mungu Yesu Kristo. Kitabu kinasema wazi kuwa fundisho hili halikuwahi kuwa katika teolojia ya kikristo mpaka kufikia karne ya nne.  Tokea maandiko matakatifu yaandikwe imepita miaka takribani 300 ndio fundisho la utatu linaingia katika kanisa. Swali la kujiuliza ni kwamba, kama hili fundisho lingekuwa ndani ya Biblia, kwanini Yesu hakulifundisha, mitume hawakulifundisha wala hatuna maandiko ya kanisa la kwanza linalosema kuwa Mungu ni nafsi Tatu. Kila mmoja ambaye akili yake ameiweka kwaajili ya kujifunza ukweli wa Biblia anatambua kuwa Fundisho la utatu ni fundisho lililotoka nje ya imani ya Yesu na Mitume na ni fundisho ambalo halipo kabisa katika maandiko matakatifu. Vitabu vya historia vinafunua ukweli kuhusu fundisho hili la kipagani, vitabu vya historia kinaweka bayana ukweli wa anzisho la utatu. Lakini kwanini leo hii historia ya fundisho la utatu haisemwi wala haijulikani? Ni kwasababu makanisa yote ya ukristo ikiwamo kanisa la waadventista wasabato hawataki watu wajue asili ya hili fundisho la kipagani. Ni kwasababu makanisa hayataki watu wa Mungu wajue ukweli. Lakini Mungu wetu hatuachi gizani lakini anaendelea kufunua kweli yote kwetu ili tutoke Babeli. Tuangalie nukuu kutoka kitabu cha kanisa katoliki inasema,

Kuanzishwa kwa ‘Mungu katika nafsi tatu’ haikuwepo hapo kabla, haikuingizwa kikamilifu katika maisha ya kikristo na katika Imani kabla ya mwisho wa karne ya nne” ( The New Catholic Encyclopedia, 1967)

Kanisa katoliki ndio lililoanzisha fundisho hili katika karne ya nne. Kama hili fundisho lingekuwa ni fundisho la kweli kwanini lisubiri miaka takribani 300 ndio likubalike kama ni ukweli wa Biblia? Kila mwanafunzi wa Kweli katika biblia anajiuliza hilo swali, kisha atatambua kuwa fundisho hili ni kama lile la kuanzishwa kwa kuabudu siku ya jumapili lilivyoingia katika imani ya kikristo wakati sio fundisho la kikristo. Kanisa katoliki ndio mwanzilishi wa Mafundisho ya uongo yaliyoyatoa katika dunia ya upagani na kuingiza katika imani ya kikristo. Kutetea mafundisho la utatu ni kutetea mamlaka ya kanisa katoliki. Kitabu cha Encyclopedia Britannica kinasema,

“Sio neno utatu wala fundisho la aina hiyo linaonekana katika Agano jipya, wala Yesu na wafuasi wake hawakujaribu kuipinga shema ya Agano la kale “ Sikiliza Ee Israel BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja ­(Kumb.6:4). Fundisho hili lilianza taratibu katika kipindi cha karne nyingi kwa kupitia mabishano  mengi. Mwishoni mwa Karne ya nne, fundisho la utatu lilichukua umbo na likabaki hivyo tokea kipindi hicho” (Encyclopedia Britannica, 1976).

Shema ilikuwa ni kauli iliyokatika Kumbukumbu la torati 6:4 ambayo ilikuwa inawakumbusha wana wa Israel kuwa Mungu ni mmoja. Yesu naye aliisema wazi shema akisema kuwa Mungu ni mmoja,

“Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, Sikia Ee Israel Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja” (Marko 12:29).

Yesu hakujaribu hata kidogo kusema kuwa Mungu ni zaidi ya mmoja ambaye ndio Baba yake kama Leo hii inavyofundishwa. Yesu alisema wazi kuwa Mungu ni mmoja tu ambaye Huyu Mungu ndiye Baba yake. Encyclopedia Britannica inasema wazi kuwa Fundisho hili halikuwepo kabisa katika ukristo mpaka kufikia katika karne ya nne. .
Baada ya kuwa tumeona asili ya utatu kuwa ni fundisho la kipagani kutoka katika vyanzo mbali mbali vya historia, Sasa tuangalie utatu wa kwanza kabisa katika historia na katika dunia ya upagani. Utatu wa kwanza kabisa ni ule utatu ambao ulikuwepo katika kipindi cha babeli baada ya gharika. Mizizi ya fundisho la utatu hivi leo linatoka katika Babeli ya kale. Katika babeli ya kale Nimrod alikuwa ndio mtawala wa taifa hilo. Nimrod alimuoa Mama yake mzazi na kuzaa naye mtoto. Kwa bahati mbaya ni kwamba wakati Nimrod anakufa alimuacha Mke wake ambaye pia ni mama yake ana mimba
Baada ya kuwa mume wake na mfalme wa taifa hilo Nimrod amefariki, Semiramis ambaye ndiye mke na mama wa Nimrod alitangaza kuwa Nimrod alikuwa ni mungu. Aliwatangazia kuwa Nimrod alikuwa anauwezo wa kimungu na ya kwamba hajafa ila amerudi tena kuishi katika utu wa mtoto wake yani Tammuz. Tukumbuke kuwa Nimrod alikufa kabla hata hajamuona mtoto wake Tammuz. Semiramis alitangaza kuwa Tammuz ndio Nimrod katika mwili mpya. Watu wa Babel wakaanza kumwabudu Nimrod na wakamwabudu Semiramis na pia wakamwabudu Tammuz.
Semiramis aliabudiwa kama ni “Mama wa mungu” na nafsi ya pili ya uungu  na Tammuz aliabudiwa kama “mungu mwana” na kama ni nafsi ya tatu ya uungu. Mwandishi John Sims anasema,

“Taratibu za utatu wa uungu inarudi nyuma katika taifa la kwanza lililokuwa linaitwa Babeli. Hii ilifanyika  kipindi cha Nimrod na Semiramis. Katika utatu huu wa kipagani wa kwanza, Mfalme Nimrod alikuwa ni nafsi ya kwanza, Semiramis malkia wake alikuwa ni nafsi ya pili na Tammuzi mtoto wao alikuwa ni nafsi ya tatu ya mungu.” (John Sims, Scriptural Harmony Process)
Mwandishi anasema kuwa Utatu unarudi nyuma katika taifa la kwanza katika historia ya ulimwengu. Utatu chanzo chake ni katika taifa la kwanza duniani yani taifa la babeli. Mwandishi anasema wazi kuwa Nimrod aliabudiwa kama ni Nafsi ya kwanza ya uungu, na Semiramis aliabudiwa kama ni nafsi ya pili ya uungu na tammuzi kama nafsi ya tatu. Tunaona kuwa utatu huu ulikuwepo kipindi cha zamani sana na watu walikuwa wanawaabudu hawa watatu kama vile ni mungu mmoja. Wa misri waliwaita Nimrod, Semiramis na Tammuz kwa majina ya kwao ambayo yalikuwa ni Osiris (Nimrod) Isis (Semiramis) na Horus (Tammuz). Osiris, Isis na Horus ni utatu wa kimisri na ulikuwepo kipindi kirefu huko Misri

Tunaona kuwa baada ya kuenea Huko babeli, fundisho hili linaendelea Huko misri na kuwa ni fundisho lao kuu. Utatu ambao chanzo chake ni babeli sasa umeamia huko Misri baada ya taifa hilo kufa. Hata baada ya kuwa taifa ya babeli kutawanyika na kufutika katika uso wa dunia lakini Fundisho la utatu halikufutika katika uso wa dunia liliendelea kuwepo huko Misri. Mwanahistoria Alexander Hislop anasema

“Ibada za sanamu ulikuwa ndio utambulisho wa Babeli wa umoja wa kimungu, ambapo Yehova Mungu aliye hai alipinga vikali sana watu wake kushiriki katika hayo.  Katika umoja wa mungu mmoja na wa pekee wa wababeli, kulikuwa na nafsi tatu na waliweka alama ya fundisho la utatu ambayo ilikuwa ni pembe tatu zilizolingana kama inavyojulikana kanisa la Roma linafanya hivyo hata leo. ( Alexander Hislop,The Two Babylons, pg. 16,17)

Mwandishi anasema wazi kuwa mtindo wa kuwa kuna Mungu mmoja katika nafsi tatu haukuanzia leo hii, bali ulikuwepo katika babeli ya kale. Wababeli walikuwa na mungu mmoja mwenye nafsi tatu kama jinsi mwandishi huyu wa historia anavyosema wazi. Wababeli walikuwa wanaabudu katika mungu mmoja mwenye nafsi tatu na kila nafsi ilikuwa ni mungu kamili. Lakini leo hii hatujui kuwa mungu mmoja mwenye nafsi tatu kwa mara ya kwanza kabisa ilifundishwa katika taifa kale zaidi duniani yani taifa la Babeli. Kanisa katoliki lilifundisha kitu ambacho kilitoka babeli ya kuwa Kuna Mungu mmoja mwenye nafsi tatu. Wababeli walikuwa ni watu wanaoabudu katika sanamu. Babeli ya sasa inafanana kabisa na ile babeli ya kale maana katika makanisa ya kanisa Katoliki, kuna sanamu za kila aina, zingine ambazo zilikuwa ni sanamu za miungu zikapewa jina la kikristo, lakini zilikuwepo hata kabla ya ukristo. Tutajifunza vyema ibada ya sanamu zilizobadilishwa jina na kuingia katika ukristo kwa kupitia kanisa katoliki. Mwanahistoria  Schulz anasema,

“Baada ya kifo cha Nimrod, Semiramis akadai kuwa mtoto wake wa kiume Tammuz alikuwa ni Nimrod aliyezaliwa tena. Osiris (Nimrod), Isis (Semiramis) and Horus (Tammuz) wakawa ni utatu wa miungu uliotukuzwa sana” (Schulz Exploring Ancient History: the First 2500 years, ch 11, 24).
Mwandishi anasema wazi kuwa baada ya kuwa Nimrod ambaye wamisri walikuwa wanamuita Osiris kufa, semiramis alitangaza kuwa mtoto wao Tammuz au aliyekuwa anajulikana kama Horus katika imani ya wamisri kuwa alikuwa ni Nimrod aliyezaliwa kama Tammuz. Watu wote katika utawala wa babeli waliwaabudu Osiris (Nimrod) Semiramis (Isis) na Horus (Tammuz) kama ni utatu wa miungu na wote waliabudiwa kama ni mungu mmoja katika nafsi tatu. Historia inajirudia kila mmoja ambaye amechunguza katika historia anatambua kuwa jambo hili ni mpango wa shetani tokea kipindi cha kale sana katika historia ya ulimwengu. Leo hii tunafikiri kuwa Mungu wa Mbinguni ni Mungu katika nafsi tatu. Lakini huyu hakuwa ni Mungu wa waisrael wala Mungu wa watu wote wanaochunguza maandiko matakatifu ya Mungu. Mungu wa babeli ndio mungu mwenye nafsi tatu, lakini Mungu katika Biblia ni Mungu ambaye ni nafsi moja tu.

Dini zote za kipagani kutoka katika wakati wa babeli, waliamini kwa namna moja au nyingine fundisho la utatu au umoja wa miungu wa tatu. Katika babeli ilikuwa ni Nimrod, Semiramis, na Tammuz. Misri ilikuwa ni Osiris, Isis na Horus. Katika Falsafa za Plato ilikuwa ni Baba asiyejulikana, logos na roho ya ulimwengu. Utatu wa kigiriki uliundwa na Zeus, Athena na Apollo. Warumi walikuwa na utatu wa Jupiter, Mercury, na Venus. Wahindi walikuwa na utatu wao wa Brahma, Vishnu na shiva.” ( Herbert Armstrong, The lost Doctrines of Christianity The doctrine of the trinity is based upon scriptures).

Mwandishi anatoa historia fupi kuhusu dini za kipagani za kipindi cha kale kabla ya kuwepo kwa ukristo. Mwandishi anasema wazi kuwa hii ilikuwa ni imani ya kipagani katika dunia ya kale. Dini zote za kipagani zilikuwa na fundisho la utatu. Hata plato katika falsafa zake alifundisha utatu lakini hakufundisha utatu mpya bali ule wa kale aliokuwa anaujua na kusikia kutoka katika dini za kipagani. Leo hii tunaona kuwa utatu upo katika makanisa yetu leo, maana yake ni kwamba upagani umefanikiwa kuingia katika imani ya kikristo hata katika imani ya kanisa la waadventista wasabato. Historia inaongea wazi kuhusu fundisho la utatu, historia ni shahidi ambaye haongei uongo bali anasema wazi kile ambacho kilitokea enzi za dunia ya kale. Msomaji na atambue kuwa wakati ni sasa wa kumwabudu Baba ambaye ndiye Mungu wa pekee wa Kweli. Tumtafute Mungu wa kweli mwenye nafsi moja tu na tumfate yeye.

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

HISTORIA YA ALAMA YA MSALABA

MUNGU ANA NAFSI NGAPI?

1YOHANA 5:8 NA MATHAYO 28:19 ZINASEMAJE?