CHINI YA SHERIA.
“Lakini
Kabla ya kuja ile Imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria tumefungwa mpaka ije
ile imani itakayofunuliwa. Hivyo torati
imekuwa kiongozi kutuleta kwa kristo ili tuhesabiwe haki kwa Imani. Lakini
iwapo imani imekuja hatupo tena chini
ya kiongozi. Kwakuwa ninyi nyote mmekuwa
wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu.”(Wagalatia
3:23-26).
Katika huu mstari kitu cha kwanza tunachoweza kujifunza ni kwamba kuja kwa
ile Imani sio kuja kwa Kristo mwenyewe, maana huwa tunafikiri kuwa
kuja kwa ile Imani ndio kuja kwa Kristo
mwenyewe hapa duniani . Mtume Paulo anasema kuwa “Kabla ya kuja ile Imani tulikuwa tumewekwa
chini ya sheria” tunafanya kosa kutafsiri kuwa “kabla ya
kuja kwa Kristo hapa duniani kwa mara ya kwanza tuliwekwa chini ya sheria”. Bali ni kabla ya Kuja kwa Imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria,
sasa swali la kujiuliza ni kwamba Imani inakujaje?
“Basi
Imani chanzo chake ni kusikia na kusikia huja kwa neno la kristo”(Warumi
10:17).
Imani inakuja kwa kusikia neno la Kristo, na neno la kristo ndilo kweli.
Hivyo basi mtume Paulo anaposema kabla ya kuja ile Imani tulikuwa tumewekwa
chini ya sheria, maana yake ni kwamba kabla hatuja sikia habari njema za
ukombozi na ukweli wa Neno la Kristo lioneshalo mapenzi ya Mungu, tulikuwa
tumewekwa chini ya sheria. Imani inakuja pale ambapo tumesikia neno la kristo
ambalo katika hilo tunafahamu Mungu wa Kweli ni yupi.. Kabla hatujasikia neno la Kristo tulikuwa gizani na vipofu, lakini
Tuliposikia neno la Kristo basi Imani ikaja kwetu. Kipindi ambacho bado tulikuwa
hatujasikia neno la Kristo tulikuwa chini ya sheria. Je kuwa chini ya sheria ni
nini?
“Lakini
Mkiongozwa na Roho hampo chini ya sheria”(Wagalatia 5:18).
Maana yake ni kwamba kama Roho sio kiongozi wetu basi tupo chini ya sheria.
Kwa hiyo kuwa chini ya sheria ni pale ambapo Roho haongozi matendo yetu na maisha yetu. Kuwa chini ya sheria ni kuongozwa na Roho wa Shetani. Hivyo wale wote walio chini ya sheria Roho wa Mungu sio kiongozi wao wapo
katika matendo ya mwili
“Basi matendo ya mwili ni dhahiri ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,
ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,
husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo katika hayo nawaambia
mapema kama nilivyokwisha kuwaambia ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo
hawataurithi ufalme wa Mungu”(Wagalatia
5:20-21).
Sasa tunapata kufahamu nini? Kuwa kabla ya kusikia neno la Kristo Imani
ilikuwa bado haijaja ndani ya Mioyo yetu, roho wa Mungu alikuwa sio Kiongozi
wetu na tulikuwa tumefungwa katika hatia ya dhambi. Torati ilikuwa inatuhukumu
kuwa sisi ni wadhambi na kifo ndio adhabu yetu. Katika kuona ubaya na hukumu
ambazo Sheria inatushikilia tunaona tukimbilie kwa Kristo ili azifute hizo
hukumu na hatia Sheria inazotushuhudia. Katika hilo basi Torati imekuwa
kiongozi ili kutuleta kwa Kristo tuhesabiwe haki kwa Imani. Ile hukumu, ile
hatia, ile adhabu ya kifo tuliyoipata baada ya kuvunja sheria inatufanya
tukimbilie kwa Kristo ilituhesabiwe haki kwa imani, baada ya kuamini kuwa katika
yeye ndipo ondoleo la dhambi linapatikana, Sasa Iwapo Imani imekuja hatupo tena
chini ya kiongozi. Kuwa chini ya kiongozi ni kuwa chini ya sheria.
Tunatambua kuwa baada ya kusikia neno la kristo liletalo uzima, na kuamini juu
ya ahadi zilizopo ndani ya Kristo ikiwamo ahadi ya Msamaha wa dhambi, basi Roho
wa Mungu anakuwa ni kiongozi wa matendo yetu na pia kiongozi wa maisha yetu. Sheria haituhukumu kuwa ni wavunjaji wa sheria tena kwa maana hatupo tena
chini ya sheria bali tupo katika sheria, tunakuwa tena sio wavunjaji wa sheria,
bali watiifu wa sheria. Maana kila aliyechini ya Sheria au chini ya kiongozi ni
Mvunjaji wa sheria. Baada ya Imani kuja ndani ya mioyo yetu sisi sio tena
wavunjaji wa Sheria bali wafataji na watiifu wa sheria ya Mungu. Katika hili tumekuwa wana
wa Mungu kwa njia ya Imani kwa Yesu Kristo. Na kama sisi ni Wana wa Mungu
kupitia Kristo, basi tumekuwa uzao wa Ibrahimu.
“Kwa
maana dhambi haitawatawala ninyi, kwa sababu hamwi chini ya sheria bali chini ya neema”(Warumi 6:14).
Katika huu mstari unaoendelea kufafanua wazi nini maana ya kuwa chini ya
sheria, walio chini ya neema dhambi haina nguvu tena kwao kwa maana Roho wa Mungu anakaa ndani yao. Bali walio chini ya
sheria dhambi ndio inawatawala kwa maana roho wa shetani anakaa ndani yao. Tunaendelea kujua kuwa, kuwa chini ya sheria ni
kutawaliwa na dhambi na roho wa Mungu sio Kiongozi wa watu hao. Bali roho wa
Mungu ni kiongozi wa wote walio chini ya neema yaani walio katika utii wa Sheria za Mungu. Msomaji asisahau kanuni hii ya
kwamba, kuwa chini ya sheria SIO KUTII AU KUFATA SHERIA, BALI NI KUVUNJA AU
KUTOKUTII SHERIA YA MUNGU. WALIO CHINI YA SHERIA ROHO WA MUNGU SIO KIONGOZI WA MATENDO YAO BALI NI ROHO WA SHETANI. Walio chini ya sheria ni wavunjaji wa Sheria. Kristo
amekuja kutukomboa sio katika kutiii sheria bali katika kuvunja sheria. Yoyote aliyechini ya sheria ni mvunjaji wa sheria na mvunjaji wa sheria anakuwa katika laana ya sheria.
Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya. Na watu wote waseme, Amina. (Kumb. 27:26)
Yesu alikuja kututoa katika laana ya sheria, na kutuokoa tutoke kuwa chini ya sheria. Kwa kutupa Roho wake atuongoze, Yesu alitukomboa tusiwe chini ya sheria. Kwa maana kuwa chini ya sheria ni kuwa katika ya laana ya torati iliyokuja baada ya kuvunja Sheria za Mungu.
Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya. Na watu wote waseme, Amina. (Kumb. 27:26)
Yesu alikuja kututoa katika laana ya sheria, na kutuokoa tutoke kuwa chini ya sheria. Kwa kutupa Roho wake atuongoze, Yesu alitukomboa tusiwe chini ya sheria. Kwa maana kuwa chini ya sheria ni kuwa katika ya laana ya torati iliyokuja baada ya kuvunja Sheria za Mungu.